Saturday, May 7, 2011

MKUTANO WA KUIMARISHA UHUSIANO JE ALIYOSEMA SHEIN YATATEKELEZWA AU NDIO KAMA MIAKA MENGINE WANASEMA KISHA HAKUNA MOJA LIFANYWALO..? TIME WILL TELL



Wajumbe wa Mkutano wa siku tatu kutoka mashirika ya kimaendeleo wakiwa katika mkutano wa kuimarisha uhusiano baina ya Viongozi wa kisiasa na kiutendaji katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, Unaoendelea katika ukumbi wa mikutano wa Zanzibar Beach Resort.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesema kuwa ili kuwaletea wananchi maendeleo yanayotarajiwa ni lazima viongozi wawe tayari na wafanye kazi wakiwa timu moja.
Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati akifungua semina ya siku tatu ya viongozi wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar pamoja na watendaji wakuu, inayofanyika katika ukumbi wa hoteli ya Zanzibar Beach Resort, Mazizini nje kidogo ya mji wa Zanzibar.
Katika hotuba yake ya ufunguzi, Dk. Shein alisema kuwa madhumuni makubwa ya semina hiyo ni kuwawezesha viongozi wanasiasa na watendaji wakuu wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuwa na mahusiano na mashirikiano mazuri zaidi ili hatimae kuwe na timu moja yenye ari kubwa ya kuwatumikia na kuwaletea maendeleo ya haraka wananchi.
Alisema kuwa pamoja na kuwa na timu imara, viongozi hao watawatumikia wananchi vizuri zaidi iwapo uchumi utakua kwa kasi kubwa na utawala bora utachukua nafasi yake ipasavyo hapa Zanzibar.
Aidha Dk. Shein alieleza kuwa semina hiyo inatoa fursa ya kukutana ili viongozi wote kwa pamoja waweze kujadili masuala mbalimbali yanayohusu maendeleo ya nchi ili hatimae viongozi hao wawe na mtazamo na mwelekeo mmoja katika kuwaletea maendeleo wananchi wote.
Alieleza kuwa wananchi wamejenga matumani makubwa kwamba Awamu ya saba ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar yenye Muundo wa Umoja wa Kitaifa itawaletea maendeleo makubwa na ya haraka na wahusika wakubwa wa kufanikisha maendeleo hayo ni viongozi hao wanasiasa na watendaji wakuu.
Katika hotuba yake hiyo, Dk. Shein alisema kuwa kukutana huko kwa pamoja kati ya viongozi wa kisiasa na watendaji wakuu wa serikali katika semina ya pamoja ni kuendeleza mkakati wa utekelezaji wa changamoto mbali mbali zilizopo katika Mawizara pamoja na kutafuta njia za kuzipatia ufumbuzi changamoto hizo.
Alieleza kuwa karibu mada zote zitakazowasilishwa katika semina hii zinauhusiano wa moja kwa moja na utendaji wa kila siku, uchumi au utawala bora.
Alisema kuwa viongozi wote wanawajibu wa kufanya kila wawezalo ili kuhakikisha kuwa uchumi unaimarika zaidi ambapo pia, unazingatia utawala bora katika utekelezaji wa majukumu yao ya kila siku.
Pamoja na hayo, Dk. Shein alieleza kuwa anamatumaini makubwa kwamba pamoja na mambo mengine, semina hiyo ya siku tatu itawawezesha viongozi hao kupata mafanikio makubwa yakiwemo kuelewa wajibu wa viongozi hao na mipaka yake katika kutekeleza majukumu yao.
Pia, alieleza kuwa viongozi hao katika semina hiyo wataelewa misingi ya uhusiano na mbinu za kukuza uhusiano na ushirikiano mzuri kati ya viongozi wa kisiasa na watendaji wakuu ambayo ni muhimu sana katika kutekeleza majukumu ya viongozi na watendaji wakuu kwa ufanisi zaidi.
Akieleza miongoni mwa mambo mengine muhimu alisema ni pamoja na kuelewa misingi ya utawala bora na umuhimu wa kuzingatia utawala bora katika utekelezaji wa majukumu ya viongozi hao.
Sambamba na hayo, Dk. Shein alisema kuwa semina hiyo itawasaidia viongozi hao kuelewa kuhusu mbinu bora za mawasiliano na umuhimu wake katika kuwaletea wananchi maendeleo ya haraka pamoja na kuelewa mafanikio mengine juu ya semina hiyo.
Dk. Shein pia, alitoa shukurani maalum kwa Sekretariat ya Jumuiya ya Madola yenye Makamo Makuu yake huko London, Uingereza na hasa ndugu Dunstan Maina kwa mashirikiano makubwa ya kufanikisha semina hiyo pamoja na kutoa shukurani kwa washiriki wote wa semina hiyo.
Nae ndugu Dunstan Maina akitoa salamu kutoka Jumuiya ya Madola alisema kuwa Jumuiya hiyo itaendelea kuunga mkono nchi wanachama wake katika juhudi zake za kuimarisha uchumi na kupambana na umasikini sanjari na kujiletea maendeleo endelevu.
Alisema kuwa juhudi kubwa zinahitajika katika kupambana na umasikini na kukuza uchumi kwa nchi za bara la Afrika.
Pamoja na hayo ndugu Maina alitoa pongezi kwa wananchi na viongozi wote wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa kuendeleza amani na utulivu nchini.

No comments:

Post a Comment