Monday, July 11, 2011

MAALIM SEIF ASEMA FUATENI SHERIA JE SMZ YENYEWE ITAFUTA SHERIA..?


 
MAKAMU wa kwanza wa Rais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amewataka viongozi wanaosimamia sheria pamoja na wananchi kwa ujumla kuzingatia utawala wa sheria, kwa kigezo kuwa ndio msingi mkuu wa haki za binaadamu.Maalim Seif ametoa changamoto hiyo leo katika viwanja vya Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar, ziliopo Miembeni Mjini hapa, katika hafla ya maadhimisho ya siku ya ‘Afisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka Zanzibar’, ambayo imetimiza miaka tisa tangu kuanzishwa kwake Julai 10, 2002.
Akizungumza na viongozi,wafanyakazi, wadau wa sheria na wanafamilia wa wafanyakazi, amesema kuwa mbali na kuwepo kwa vyombo vya kusimamia utoaji wa haki na kuwepo wataalamu wa sheria, lakini kuna nyakati wataalamu hao hutumia matatizo au fursa ziliopo katika ushughulikiaji wa kero za wananchi kisheria, kwa manufaa binafsi au kujineemesha.
Aliwataka wadau wote kutokutoa mianya na kuruhusu baadhi ay watu wachache kutumia ujuzi au uwezo walionao kuvuruga haki za walio wengi.Aidha aliwataka wananchi, viongozi wa serikali na taasisi zake zikiwemo zile zinazosimamia sheria kutoa mashirikiano ya kutosha kwa Afisi hiyo, ili kuleta ufanisi katika kazi zake na kutimiza wajibu mkubwa wa kulinda haki katika masuala ya jinai.
Hata hivyo Maalim Seif alisema ili wananchi watimize wajibu huo na kuvitumia ipasavyo vyombo vilivyowekwa, kuna umuhimu wa kuelimishwa kikamilifu kuhusiana na taratibu nzuri za kushughulikia masuala ya jinai.
Alibainisha kuwa pale wananchi watakapobaini kuonewa, kukatishwaa tamaa au kukosa imani na vyombo vinavyosimamia haki, kuna hatari ya kujichukulia sheria mikononi mwao.Alisema kuna nyakati wananchi hukabiliana na matatizo ya kudai haki, hali inayotokana na vyombo husika kutokuwa makini na kuruhusu uonevu,hivyo alitoa wito kwa vyombo vya kisheria kutokutoa mwanya kwa wananchi kujichukulia maamuzi ya kisheria mikononi mwao.
Akigusia umuhimu wa kuwepo kwa Afisi ya mkurugenzi wa Mashtaka, Maalim Seif alisema imekuwa ni kichocheo muhimu cha kukuza Utawala wa sheria ambamo ndani yake imepelekea ukuaji wa wa sekta mbali mbali,zikiwemo za kiuchumi,kisiasa,kiutamaduni na kijamii.
Alieleza kuwa wananchi wengi wameridhika na kutambua kuwa masuala ya jinai yanaendeshwa kiraia badala ya kushughulikiwa na Polisi ambao wamebaki na jukumu la kufanya upelelezi.Aidha alisema amefarijika sana kuona Afisi hiyo imejenga kituo cha mafunzo na utafiti wa sheria, ambacho kinategemewa kuanza kufanyakazi mwaka huu.
Alibainisha matumaini yake kuwa mafunzo yatakayotolewa yatainufaisha jamii ya Afrika, na kutoa wito kwa viongozi na wananchi wote kukitumia kituo hicho ili Taifa liweze kutoa wataalamu mbali mbali katika fani tofauti.
Mapema Waziri wa Katiba na Sheria Zanzibar, Abubakar Khamis Bakari, alisema mbali na mafanikio makubwa yaliofikiwa tangu kuanzishwa kwa Ofisi hiyo, bado kuna upungufu wa Waendesha Mashtaka katika ngazi za Mahakama za Wilaya.
Alisema mashirikiano yanahitajika miongoni mwa vyombo vinavyosimamia sheria, ikiwemo Mahakama, Polisi na wananchi ili kufikia lengo la kulinda haki za raia.
Alitumia fursa hiyo kumpongeza muanzilishi wa Afisi hiyo Othman Masoud, ambae kwa sasa ameteuliwa kuwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa juhudi, umahiri na kuwa na dira iliowezesha ofisi hiyo kupata mafanikio makubwa ndani ya kipindi kifupi, kiasi cha kutoa ushindani kwa taasisi nyengine za aina hiyo ziliomo katika Jumuiya ya Afrika Mashariiki.

maana SMZ imenyaganya mashamba ya watu nyumba za watu na nakuvitaifisha sasa kama sheria imekuja tuanze kwenye shina na shina la mathambi haya yote yanayotokeya znz maalim ni SMZ ambayo imeficha makucha yake na kutenda mambo mengi chini kwa chini siku hizi maana wanaogopa sasa tuwaa anze wao hao wabunge na mawaziri waliyonyanganya watu mashamba yao wayarudishe na nyumba za mji mkongwe zilizo geuzwa ofisi za SMZ warudishiwe wenyewe labda babu zao washakufa ila wajuku wako kisha safisha serekali basi wananchi ni rahisi kufuata maana watajuwa sasa serekali yetu haina mzaha lakini kama sio hivyo itakuwa kama unampigia mbuzi gita unasubiri acheze wala hachezi anakula tu majani.

No comments:

Post a Comment