Tuesday, August 9, 2011

VIBANDA VYA VINYAGO VYATEKETEA NCHINI ZANZIBAR


Imeandikwa na Khatib Suleiman, Zanzibar; Tarehe: 8th August 2011 VIBANDA 30 vya wafanyabiashara wa bidhaa za utalii ikiwemo vinyago vilivyopo Kiwengwa Mkoa wa Kaskazini Unguja vimeteketea kwa moto.
Kamanda wa Polisi wa Mkoa huo, Mselem Mtulya alisema wanachunguza tukio hilo.“Ni kweli vibanda vya biashara vya vinyago vimeteketea lakini kwa sasa tunafanya uchunguzi kujua chanzo chake … ufupi inaonekana vimechomwa moto kutokana na ugomvi binafsi wa kimapenzi,” alisema Mtulya.Alidai ugomvi huo uliwahusisha Mrisho Suleiman Pandu na Amina Ali na baadaye Mrisho alidaiwa kuchoma moto kibanda hicho wanachoishi na kuharibu vibanda vyengine.Polisi inamshikilia Pandu kwa kufanya uhalifu wa uchomaji moto kibanda wanachoishi na anatarajiwa kufikishwa mahakamani leo.Mkuu wa Wilaya ya Kaskazini Unguja, Vuai Ali Vuai alifika katika eneo hilo na kuwataka wahusika kusitisha ujenzi wa vibanda vipya kwa sasa.Alisema ujenzi wa vibanda vipya lazima uhusishe halmashauri ya wilaya kwa ajili ya upimaji wa eneo hilo na kupata ramani ili wajue mahitaji mbali mbali muhimu.“Nimeagiza kusitisha mara moja kwa ujenzi wa vibanda vipya vya biashara katika eneo hilo hadi halmashauri ya wilaya ipime na kujua mahitaji ya wananchi,” alisema Vuai.
Alisema vibanda vilivyoteketea kwa moto vimejengwa kiholela na kuezekwa kwa makuti ambayo ni rahisi kushika moto na kuteketea.Vuai alisema eneo hilo kwa sasa linahitaji majengo ya kudumu ambayo yatazingatia mahitaji yote muhimu ikiwemo vyoo na maeneo ya chakula.Zaidi ya wafanyabiashara 50 wameathirika na moto huo na kwa sasa wamesitisha biashara zao katika eneo hilo.Hii ni mara ya nne kwa vibanda vya eneo hilo vikiwemo vya vinyago na mama lishe kuteketea kwa moto.

No comments:

Post a Comment