Monday, August 6, 2012

KOMANDO MANSOOR YUSSUF HIMID AKUMBUSHIA KITI CHA U.N


Waziri Mansoor aunga mkono mkataba!
Waziri wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar (SMZ), Mansoor Yussuf Himid, amependekeza kuwepo na Muungano wa mkataba kati ya Tanzania bara na Zanzibar.
Mansoor alitoa matamshi hayo wakati akichangia hoja kwenye semina ya mjadala wa mchakato wa ukusanyaji maaoni ya uundwaji wa Katiba mpya ya Jamhuri ya Muugano Tanzania uliofanyika katika ukumbi wa Baraza la Wawakilishi Chukwani Zanzibar.
Alisema ipo haja ya kuwa na Muungano wa mkataba ili kuondokana na malalamiko mengi ambayo yanalalamikiwa katika Muungano wa sasa.
Katika maelezo yake, Mansoor alisema bado ataendelea kuwa muumini wa mfumo wa serikali mbili chini ya mkataba na si kama ilivyo sasa ili kuipa fursa zaidi Zanzibar kujijenga na kujitegemea kiuchumi.
Alisema si dhambi Zanzibar na Tanganyika chini ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania zote zikawa na viti viwili katika Umoja wa Mataifa (UN).
Alieleza kuwa kuna baadhi ya viongozi kwa malengo yao binafsi wanajaribu kuwajengea hofu wenzao na kuwazuia kutoa maoni yao kwa upana kama raia huru kwa mujibu wa Katiba ya nchi.
Aliongeza kuwa hajawahi hata mara moja kukataa Muungano, ila mara zote amekuwa akihimiza mabadiliko ya kimfumo katika Muungano huo na kwamba anaamini kuwa kufanya hivyo si uadui wala usaliti.
“Hata NEC ya CCM ilipoanzisha mchakato wa Serikali ya Umoja wa Kitaifa kulienezwa hofu kila mahali, nashukuru tumefanikiwa kuunda GNU, sasa imesimama na kusomga mbele, kila mmoja anaona fahari, faida na tija ya jambo hilo,” alisema.
Hata hivyo, kauli ya Mansoour ya kutaka Muungano wa mkataba na suala zima la kila upande kuwa na kiti UN, inamaanisha kwamba Zanzibar inapaswa kuwa huru.
Alisema awali suala la kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa lilipoibuliwa na Rais Jakaya Kikwete, kulikuwa na mtazamo hasi kwa baadhi ya wanasiasa waliokuwa wakiamini kuwa kuundwa kwa GNU kungetoa mwanya wa kuwarejesha watawala waliopinduliwa Januari 12,mwaka 1964 na kulipizana visasi.
“Hata wenzetu wa CUF kabla ya GNU, walikuwa wakipinga kila kitu kizuri cha SMZ, baada ya kushirikishwa serikalini hata yale waliyokuwa wakiyapinga wakati ule, sasa wanayaunga mkono, kuyasimamia na kuyashangilia,” alisema Waziri Mansoor.
Akizungumzia umuhimu wa dhana ya Muungano alisema hapendi uvunjike na kwamba mara zote amekuwa akitaka hoja na haja ya Muungano huo kufanyiwa marekebisho ya msingi na kuwa chini ya mkataba.
Waziri huyo wa SMZ ambaye pia ni Mwakilishi wa Jimbo la Kiembesamaki kwa tiketi ya CCM, aliongeza kuwa ikiwa maoni yake yatachukuliwa na chama chake kuwa ametenda dhambi, atakuwa tayari kukabiliana na adhabu yoyote atakayopewa.
“Niko tayari kuadhibiwa kwa kutoa maoni ninayoyaamini kama ni ya kujenga, nafikiri nimetumia haki yangu ya Kikatiba na kiraia, nataka Zanzibar iwe na nyenzo zake za kiuchumi kwa maendeleo ya watu wake, sijali na wala sitawasikiliza wanaoeneza maneno ya uzushi,” aliongeza Waziri Mansoor.
Alisema kila Mzanzibari anayo haki ya kutoa maoni yake bila mtu mwingine kuzuia utashi wake huku akisisitiza kuwa hiyo ndiyo demokrasia anayoijua yeye ndani ya chama chake.
Hata hivyo, aliipongeza CCM kuwa ina mwelekeo, viongozi wake wana uwezo wa kuvumiliana na kupima mabadiliko ya nyakati.
“Ninakiheshimu sana chama changu, ninakipenda, ndicho kilichonilea, bado ni imara sana, kuna watu wanataka kukichafua, kufika kwetu hapa ni kutokana na utashi wa viongozi wake kuwa na dira na uvumilivu,” alisema.

No comments:

Post a Comment