Wednesday, May 15, 2013

KUNAMPANGO WA KUMUONGEZEA J.K.KIKWETE MUDA KUWA RAISI WA TANGANYIKA NDIO MAANA KATIBA MPYA INAHARAKISHWA IMALIZIKE HARAKA KABLA YA UCHANGUZI WA 2015


Dar es Salaam. Mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), Profesa Ibrahimu Lipumba amedai kuwa amenasa taarifa za siri za kuwapo kwa mipango ya kuongeza muda wa Serikali ya sasa kukaa madarakani TENA.
Profesa Lipumba alisema hiyo inatokana na wasiwasi kuwa mchakato wa Katiba Mpya hautaweza kukamilika mwaka 2014 hivyo kutokuwa rahisi kwa uchaguzi kufanyika mwaka 2015.
Akizungumza Dar es Salaam jana, wakati akifungua kikao cha Baraza Kuu la CUF, Profesa Lipumba alisema kuwa Serikali inataka kuongezewa muda wa kukaa madarakani kwa miaka miwili ikimaanisha kuwa Serikali ya Awamu ya Nne chini ya Rais Jakaya Kikwete itakaa madarakani hadi mwaka 2017.
Hata hivyo, madai hayo ya Profesa Lipumba yamepingwa vikali na Serikali na viongozi wake watatu waandamizi ambapo walijibu walipoulizwa kwa maandishi na wandishi tafauti akiwemo muandishi wetu wa siri mjini Dodoma wanakohudhuria kikao cha Bunge.
Waziri wa Katiba na Sheria, Mathias Chikawe alijibu: “Mchakato wa Katiba upo ‘on track’ (unakwenda vizuri) hatuna sababu ya kufanya hivyo.”
Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Jaji Frederick Werema alijibu” “Njooni ofisini kwangu nitasema ni kitu gani.”
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, Sera, Uratibu na Bunge, William Lukuvi alijibu kwa utani bila ya kufafanua: “Njooni niwajuze, unajua kamba haitoki Ukambani kama ilivyo kamba.”
Profesa Lipumba amemwomba Rais Kikwete asilikubali wazo hilo akisema wananchi hawatakubali na taifa linaweza kuingia katika mtafaruku.
“Nitapenda kuona Rais Kikwete akikataa jambo hilo kwani litachafua taswira ya nchi. Hatua hii ni kinyume cha utawala bora,” alisema Profesa Lipumba.
Alisema Serikali haipaswi kuhofia uchaguzi kwa sababu ya Katiba kwani bado uwezekano wa kuandaa uchaguzi wa haki na huru unawezekana kwa utaratibu mwingine.
“Mchakato wa Katiba unaendelea, Tume ya Mabadiliko ya Katiba inatuambia kwamba mwaka 2014 tutakuwa na Katiba Mpya, sasa CUF tunasema kwamba hata kama Katiba Mpya haitapatikana kwa kipindi hicho kuwe na Tume huru ya Uchaguzi,” alisema Profesa Lipumba.
Jukwaa la Katiba kutinga mahakamani
Siku nne baada ya Tume ya Mabadiliko ya Katiba kutoa rasimu ya mwongozo kuhusu uundwaji wa Mabaraza ya Katiba, Jukwaa la Katiba nchini Tanganyika (Tanzania) (Jukata), limesema litafungua kesi mahakamani kutaka kusitishwa kwa mchakato mzima wa Katiba Mpya kwa madai kuwa uendeshwaji wake umejaa mizengwe, itikadi za vyama na rushwa. Limetaja sababu tano ambazo zimekiukwa.
Limesema kesi hiyo itasimamiwa na timu ya mawakili 10 watakaoongozwa na Mwanasheria wa masuala ya Haki za Binadamu, Dk Rugemeleza Nshala na itawasilishwa mahakamani siku saba zijazo kuanzia jana.
Akizungumza na waandishi wa habari Dar es Salaam jana, Mwenyekiti wa Jukata, Deus Kibamba alitaja sababu hizo kuwa ni kutokufanyiwa marekebisho katika sehemu tatu za Sheria ya Mabadiliko ya Katiba kama ilivyoahidiwa na Rais Kikwete, kuvurugwa kwa Uchaguzi wa Mabaraza ya Katiba, mchakato wa Katiba kukosa uongozi, kuminywa kwa demokrasia wakati wa mchakato huo pamoja na Jukwaa hilo kuzuiwa kuonana na Rais ili kueleza upungufu uliopo.

1 comment:

  1. Tutakuwa na katiba mpya 2014. Si kweli Kikwete anataka kuwa raisi mpaka 2017 kama Ibrahim Lipumba, CUF, alivyosema. Tatizo la katiba mpya ni kwamba haitakuwa na kifungu kitakacho waruhusu Wazanzibari kujitenga, siyo kwamba haitakubaliwa. Raisi Kikwete anastahili sifa na heshima. Atakumbukwa katika historia ya Tanzania kuwa ni raisi wa kwanza aliyewaruhusu Watanzania kuwa na katiba yao wenyewe, katikba mpya ambayo imejadiliwa na kukubaliwa na wananchi. Haijawahi kutokea katika historia yetu. Kabla ya hapo, katiba zote zilikuwa na za chama tawala na wabunge wake. Pia Kikwete atakumbukuwa kuwa ni raisi aliyewaruhsu Watanzania kuwa na uhuru wa kusema na kuandika wanachotaka magazetini na mtandaoni. Hata wanapomshambulia sana na kumtukana Jamiiforums, anavumilia. Mkapa angekuwa raisi, msingekuwa na Jamiiforums. Lipummba, badala ya kumlaumu Kikwete, atafute njia itakyowapa Wazanzibari haki yao ya kujitenga.

    ReplyDelete