Sunday, June 9, 2013

ATAKAYE NA ASIYEUTAKA MUUNGANO NANI WA KUIHAMA NCHI YA ZANZIBAR..???


jumbe-472x420
Ninashangaa sana pale mtu anaposimama hadharani na kutamka Ásiyetautaka Muungano na ahame.Ninashangaa kwa sababu,kwanza ,hapa Zanzibar hadi sasa hakuna au kundi la watu rasmi lililotangaza kuwa haliutaki muungano na msemaji wa hayo maneno analijuwa hilo,anachojaribu ni kuupindisha ukweli.
Wanachokitaka hao wanaoambiwa hawautaki muungano kiko bayana kabisa. Bali inawezekana sana kupuuzwa kwa ndiko kunaweza kuwahamisha walipo na kuwapeleka huko kwenye kuukataa kabisaaaa.
abu-ajmal1-219x300
 Na Abu Ajmal
Pili, iwapo tuna dhamira ya kweli ya kuwafahamu wanaoutaka muungano na wasioutaka muungano ili tuwaambie au kuwaagiza wahame kama anavyofanya “kichwa”, basi njia ni rahisi: sheria inampa yeye mamlaka ya kuitisha kura ya maoni. Baada ya zoezi hilo tutakuwa tumeshawajuwa wale wasioutaka. Hatuna njia nyengine ya kuwabaguwa wawili hawa zaidi ya hiyo. Vyenginevyo, tutaishia kwenye hisia tu.
Na, tatu, itakuwa inastahiki zaidi kwa wale wanaoutaka Muungano kuhama na kuufuata wao huko uliko, yaani Tanganyika. Hii kwa sababu, hawa wasioutaka Muungano hapa Zanzibar ndio kwao, na hawana pengine pa kwenda, hasa kwa vile hawautaki Muungano. Hivyo, sidhani kama watapokelewa kwengineko.
Ukweli wa mambo ni kuwa Wazanzibari wamekuwa wakidai Muungano wa heshima manufaa kwa walioungana. Muungano utakaoimarisha upendo na haki kwa wote. Na hayo sio madai mapya, yamesemwa na yameandikwa, (rejea “The Partnership” cha Aboud Jumbe Mwinyi).
Tatizo liliopo ni kwamba mshirika mmoja wa Muungano kujisikia kuwa ni “Mkubwa” na kumuona mwengine kuwa ni “Mdogo”. Anajifanya kusahau kuwa Zanzibar ni nchi kama ilivyo Tanganyika bila ya kujali udogo wake na idadi ya watu wake.
Wanaotamka hawautaki ni ishara ya tu ya kuchoshwa na kutosikilizwa kwa madai yao. Hasa unapozingatia ukweli kwamba hatua zinazoonekana stahiki kwa wale wanaokosowa jinsi Muungano huu unavyoendeshwa ni kuwaadhibu badala ya kuzingatia na kufanyia kazi matakwa yao ambayo ni wazi yana maslahi kwao na kwa kizazi kijacho.
Mmoja wa waasisi wa Muungano huu, Marehemu Julius Nyerere, alipata kusema wakati wa “kung’atuka” kwake kuwa wao kama wanadamu wamefanya mazuri na ya kijinga, hivyo akawaomba Watanzania kushika mazuri na kuachana na ya kijinga.
Wazanzibari wengi wameshaona kuwa Muungano tulionao ni katika hayo mambo ya kijinga. Sasa kwa nini tusijipe nafasi ya kufikiria Muungano utakaofurahiwa na wote? Wanaoshughulika kutatua kero hadi sasa hawajafanikiwa na hawatafanikiwa kwa kuwa wanashughulika na matokeo badala ya chanzo. Suala sio kero za muungano, bali Muungano wenyewe ndio kero.
Mwisho, ningelipenda kutoa angalizo kwa “Kichwa”: Kama kweli anamaanisha kwamba asiyeutaka Muungano huu ahame Zanzibar, basi aanze nyumbani kwake kwanza kuhamisha watu, maana tunajuwa kuwa wapo watu aina hiyo ndani mwake.
Asitoe kibanzi kilicho ndani ya jicho la jirani yake wakati jichoni mwake mna boriti. Haipendezi hata kidogo kwa mtu wa nafasi yake kutamka maneno hayo.

Mwandishi: Abu Ajmal

Mhariri: Mohammed Ghassany

No comments:

Post a Comment