Thursday, November 20, 2014

VIONGOZI WAKIUMWA WANAENDA KUTIBIWA NJE YA NCHI RAI KUFANI KATIKA MAKABWELA MPAKA LINI..??




KWA muda mrefu sasa, baada ya kila muda mfupi, tumesikia kiongozi mmoja wa nchi ya Kiafrika baada ya mwengine, amekwenda nje ya nchi yake kuchunguzwa afya au kupata matibabu. Wengi wao, wamefia huko na wengine, kama Leopold Sedar Senghor wa Senegal baada ya kutoka madarakani waliamua kuishi Ulaya haswa na walipoiaga dunia ndipo maiti zao zikarejeshwa nchini kwao kwa mazishi. Senghor ambaye alikuwa na mabilioni ya dola katika mabenki ya Ulaya na majumba katika nchi za Ulaya aliishi Ufaransa na kufia huko. Alipoulizwa kwa nini hakubaki Senegal baada ya kustaafu kuongoza nchi hio kutoka 1960 hadi 1993, alisema hakuna mtu asiyependa maisha mazuri na Afrika bado haijaendelea. Siku hizi ni kawaida ukiona Rais au Waziri Mkuu wa nchi ya Kiafrika amefika hospitali, basi ni kuangalia mgonjwa au kwa shughuli za kiserikali na sio matibabu, kama vile hospitali hizo haziwahusu au wao ni marufuku kutibiwa hapo.
Hata viongozi waliojigamba kuwa wazalendo wakubwa na kujinata kuwa chini ya uongozi wao nchi zao zilipata maendeleo makubwa katika sekta ya afya walikimbilia nje ya nchi kwa matibabu. Wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema sababu kubwa za watu hawa kufanya hivyo ni mbili. Moja ni hofu ya usalama wao kutokana na kutoamini madaktari wazalendo na nyingine ni huduma duni znazoambatana na ukosefu wa vifaa na dawa katika hospitali hizo. Kwa maana nyengine hospitali hizo zimejengwa kwa mkabwela tu kama vituo vya afya vya daraja la chini na hazina sifa za kuitwa hospitali wala kutibu wanadamu unaweza ukasama hivyo. Ni aliyekuwa Rais wa Afrika ya Kusini, Nelson Mandela, licha ya hali yake kuwa mbaya, ndiye pekee hakupelekwa nje ya nchi na alipata matibabu Afrika ya Kusini hadi alipofariki.
Lakini wengine wamekuwa siku zote kiguu na njia kwenda nje ya nchi zao kupata matibabu na kuwaacha makabwela wategeemee huduma mbovu za matibabu ziliopo nchini kwao na kwa uhakika hakuna haswa hizo huduma ni majengoo tu yapo yapo na jina kumbwa HOSPITALI lakini sio ya kuitwa hospitali hata chembe.Hebu tuanze na Marisi kidogo Rais wa Guinea, Ahed Sekou Toure, aliyekuwa akisifu huduma za afya nchini kwake tokea kupata uhuru, alikimbizwa Marekani mwezi Machi 1984, wakati akiwa na miaka 62, kupata matibabu. Alifarikia miaka 26 baadaye, lakini wakati wote alikuwa akitibiwa Saudi Arabia, Ufaransa au Marekani. Katika mwaka 2005, baada ya kutawala kwa mkono wa chuma kwa miaka 38, Rais Gnassingbe Eyadema wa Togo, alifarki akiwa ndani ya ndege iliokuwa inampeleka nje ya nchi kwa matibabu. Zilikuwepo taarifa kuwa alikuwa ameshakata roho alipopakiwa kwenye ndege lakini akapelekwa hivyo hivyo.
Katika mwaka 2008, Rais Levy Mwanawasa wa Zambia, akiwa na miaka 59, alifariki akiwa kwenye matibabu nchini Ufaransa. Naye Rais Lansana Conté (74) wa Guinea, alifariki mwaka huo huo nchini kwake muda mfupi tu baada ya kurudi kwenye matibabu Uswisi akiwa na shehena za zawadi kwa wana familia na rafiki zake. Rais Omar Bongo wa Gabon alifariki mwaka 2009 akiwa kwenye matibabu Hispania akiwa na miaka 73. Aliitawala nchi hio yenye utajiri mkubwa wa mafuta kwa miaka 38. Alichojali zaidi ni kujijengea Ikulu za fahari na ndege za kisasa na kuhakikisha mwanawe anamrithi uongozi imekuwa mafuta ya nchi ni yake yeye na familia yake sio wananchi wote. Katika mwaka 2010, Rais Umaru Musa Yar’Adua wa Ngeria alifariki akiwa na miaka 58 nchini kwake muda mfupi baada ya kurejea kwenye matibabu yaliyochukua miezi miwili nchini Saudi Arabia.
Rais John Atta Mills wa Ghana alifariki nchini kwake akiwa na miaka 68 wiki chache baada ya kurudi kutoka Marekani alipokwenda kwa matibabu. Naye Rais Bingu wa Mutharikia wa Malawi aliiga dunia miaka miwili iliopita akiwa na miaka 78 katika jiji la Lusaka, Zambia. Kabla ya hapo alikuwepo Afrika ya Kusini kwa matibabu. Rais wa Ethiopia, Meles Zenawi, naye alifariki miaka miwili iliyopita akiwa na miaka 57 wakati akiwa Ubelgiji kwa matibabu ambapo alikuwa akienda mara kwa mara na kundi kubwa la mawaziri na wasaidizi wengine ati nakwenda matibabu huyu. Novemba 2012, Guinea Bissau ilipokea maiti ya Rais wake aliyefariki katika hospitali moja ya matajiri nchini Ufaransa. Hivi kribuni tu, Rais Michael Sata wa Zambia, alifariki akiwa London kwa matibabu. Hapo kabla alitibiwa Afrika ya Kusini na India.
Orodha ya viongozi wa nchi ya  Tanganyika na  nchi yetu ya Zanzibar, waliopo madarakani na waliostaafu, wanaokwenda nje kwa matibabu mara kwa mara ni ndefu mno. Hivi karibuni tu Rais Jakaya Kikwete wa nchi ya Tanganyika naye alikuwepo Marekani kwa matibabu ya upasuaji wa tezi dume. Naye Rais Abdelaziz Bouteflika wa Algeria hivi sasa anapata matibabu nchini Ufaransa. Bouteflika ambaye sasa ana miaka 77 alipata ugonjwa wa kiharusi mwaka jana na amekuwa akitembea kwa kutumia kigari. Vile vile anazungumza kwa tabu na mara husahau alilolisema dakika chache zilizopita lakini kingngnizi bado aupenda Uraisi na yuko nje akipatiwa matibabu. Bouteflika aliwafukuza wasaidizi wake wote waliomshauri aachie uongozi baada ya kuugua ugonjwa wa kiharusi kwa madai kuwa anao uwezo mkubwa wa kuendelea kuwatumikia wananchi wa Aligeria. Alisema wale waliomshauri apumzike hawakuwa wanaitakia mema Aligeria kwa hiyo akawapumzisha wao.
Kwa kweli hali hii iliyopo hapa chini na katika nchi zote za Kiafrika za viongozi wake kwenda nje kwa matibabu, isipokuwa Afrika ya Kusini, unaweza kusema ni ya aibu. Hii inatokana zaidi na kwamba nchi nyingi za Kiafrika zimetimiza zaidi ya nusu karne tokea kupata uhuru. Hakuna takwimu sahihi ya kiwango cha fedha ambacho viongozi wa nchi za Kiafrika hutumia kwa matibabu nje ya nchi zao, lakini ukweli ni kwamba laiti fedha hizo zingetumika kuimarisha hospitali za nchini kwao, wananchi wengi wangelifaidika na huduma bora za afya. Kinachoonekana na baadhi ya wachambuzi wa mambo ya kisiasa ni kwamba viongozi wengi wa Kiafrika wanajali zaidi afya zao na zile za familia zao na sio za wananchi kwa jumla. Katika nchi nyingi za Kiafrika hivi sasa, pamoja na nchi ya Tanganyika na nchi ya Zanzibar, tunasikia malalamiko ya upungufu mkubwa wa dawa na vifaa vya kisasa vya matibabu. Hata hizo fedha kidogo zinazotolewa kwa sekta ya afya huliwa na wajanja na sio kawaida kuona mafisadi wanaohusika kuwajibshwa kisheria.
Hapana takwimu sahihi za kila nchi inatumia kiasi gani kutibu viongozi wake nje, lakini wachambuzi wa mambo ya kisiasa wanasema ni fedha nyingi sana na kwa kiasi fulani ziaongeza umaskini katika nchi hizi za Afrika. Kinachoonekana kupewa umuhimu na viongozi wengi wa nchi za Kiafrika ni kutumia fedha nyingi kwa ulinzi ili wakae milele madarakani au hata kama sio milele lakini akae madarakani japo kuwa rai hawamtaki na hawakumpigia kura, sherehe zisiokwisha za upozi mtupu na safari za viongozi nje ya nchi kila kukicha. Baadhi yao wanatumia muda mrefu zaidi nje ya nchi zao kama vile wafanyavyo marubani wa ndege za kimataifa. Hali hii ya kupuuza sekta ya afya inakwenda sambamba na kutojali kiwango cha elimu. Matokeo yake ni kwamba watoto wengi wa viongozi wameamuwa wawasomeshe Ulaya, India, Marekani na Canada maana wanajuwa kuwa nchini hakuna skuli ni midabwada tu. Wakati umefika kwa nchi za Kiafria, ikiwa pamoja na nchi ya Zanzibar na nchi ya Tanganyika, kufanya tathmini itakayosaidia kuimarisha sekta ya afya na hata viongozi nao wachunguzwe afya zao na watibiwe katika nchi zao hapana tena kwenda Ulaya wa India wala Marekani wa Canada kama wao hataki makabwela ni sisi pia hatuyataki.
Vinginevyo, raia wa kawaida naye kila anapohitaji kuchunguzwa afya yake au kupata matibabu naye apelekwe nje ya nchi na hospitali zetu zibakie kuwa mapambo ya miji yetu au kama majumba ya makumbosho tu. Wakati tunaelekea kwenye uchaguzi mkuu wa mwaka 2015 moja ya ajenda inayofaa Wazanzibari na Watanganyika kuishikia bango ni vipi hao wanaogombea urais wataimarisha sekta ya afya. Vile vile watakiwe kutoa ahadi kwamba watachunguzwa afya zao na kupatiwa matibabu hapa hapa nchini. Wale wanaotaka kwenda nje kwa matibabu watumie fedha zao wenyewe kutoka katika mishahara yao au mifukoni mwao na watoto wao wote wasome hapa hapa nchini na sio pesa  za walipa kodi.
Tukiamua inawezekana.

KILA MZANZIBARI ATAULIZWA SIKU YA KIYAMA NA MWENYEZI MUNGU ULIPOSIKIA WAZANZIBARI WENZIO WANADHALILISHWA NA KULAWITIWA NA HAWA JE ULIFANYA NINI TAFUTA JIBU LAKO MAPEMA KWA SIKU HIYO YA KIYAMA SIKU AMBAYO MALI NA WATOTO WAKO WALA CHEO CHAKO HAVITAKUFAA SIKU HIYO.

No comments:

Post a Comment