Thursday, March 12, 2015

NATOKA CCM KWANI SI MAMA NA SITAJUTIA UAMUZI HUYU NI MTANGANYIKA.JE WAHAFIDHINA,WASAKA TONGE,MADALALI WA KUTAKA KUIUZA NCHI YA ZANZIBAR CCM WAZENJI MNASEMAJE....???

Chama-Cha-Mapinduzi
Tanganyika (TANZANIA) yetu ipo njia panda. Tuliyonuia kuyafanikisha miaka 50 iliyopita, yamekwama. Na hatua tuliyopiga kama taifa haifanani na umri mkubwa wa kujitawala kwetu wala na utajiri wa rasilimali uliotamalaki kwenye ardhi yetu.Mikakati, sera na mipango mingi vimeshindwa kuwapatia watu wa taifa hili faraja wanayoistahili. Tunahitaji kuutafuta uhuru mpya wa taifa letu! Uongozi ni kuonyesha njia. Nilipokuwa mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Mbunge wa Jimbo la Kishapu kupitia chama kilichopewa dhamana ya kuongoza nchi hii kwa miaka 50, niliyashuhudia mengi ya kushtusha kuhusu mustakabali wa taifa hili. Nafsi yangu imewiwa kueleza yale niliyoyashuhudia nikiwa ndani ya mfumo wa chama na serikali ya CCM uliotazamiwa utuongoze kuifikia ile ndoto ya uhuru – ndoto ya kushinda umaskini, ujinga na maradhi.Ikiwa bado kuna Mtanzania anayeamini kwamba ndoto hiyo inaweza ikatimizwa kwa uongozi na mfumo wa utawala wa CCM tulio nao, basi uzoefu na ushuhuda wangu ukawe jibu kwake. Ikiwa bado kuna Mtanzania aliyekata tamaa, asiyeamini kwamba taifa hili siku moja linaweza kuendelea mfano wa (au hata kuzidi taifa la) Marekani na nchi za Ulaya ya Magharibi, basi rai yangu kupitia makala hii inaweza kumhakikishia jinsi inavyowezekana kufanya yale yaliyoshindikana au kusuasua kwa muda mrefu.Katika makala hii nimeona ni vyema niwaeleze wasomaji sababu zilizonifanya nihame CCM.Nianze kunukuu tamko nililolitoa kwenye vyombo vya habari, Machi 30, 2010 jijini Dar es Salaam siku nilipohama CCM;“Nimeishi kwa matumaini kwa muda mrefu, nikitegemea siku moja mambo yatabadilika ndani ya CCM, mpaka leo sioni dalili, ni heri niheshimu dhamira yangu kama Mwalimu Nyerere alivyotuasa kwamba CCM si mama yangu. “Nasononeka CCM imegeuka gulio la kila mtafuta cheo na utajiri haramu. CCM imegeuka kimbilio la kila mwenye dhamira ya ulanguzi. CCM imepoteza maadili ya uongozi na imekuwa ngome ya mafisadi wanaotafuna utajiri wa nchi yetu. “Najua Watanzania wengi sana wakiwemo wabunge wenzangu, wanasiasa wakongwe, viongozi wa dini zote, na asasi mbalimbali, waandishi wa habari, wanafunzi wa sekondari za kata na vyuo vikuu ambao vilevile nguvu ya kuendelea kuishi kwa matumaini imeisha kabisa, lakini wanasita kufanya maamuzi magumu. Siwasukumi kufuata maamuzi yangu ila nawasihi wamuombe Mungu na wasikilize dhamira zao. Natoka CCM, CCM siyo Hellena (sio mama yangu), na sijutii uamuzi wangu”.
Ni dhahiri kwa Watanzania wengi kwamba utawala wa Rais wa Awamu ya Nne, Jakaya Mrisho Kikwete, umefikwa na misukosuko mikubwa kutokana na ufisadi uliodhihirika zaidi mwanzoni mwa mwaka 2006. Mijadala mingi bungeni, kwenye vyombo vya habari na ndani ya chama tawala – CCM na vyama vingine vya siasa, imekuwa ikihusu ufisadi na rushwa ambao umesababishwa na kuporomoka kwa maadili. Kashfa za akaunti ya escrow, Richmond, Dowans, ununuzi wa rada, ubinafsishaji holela wa Shirika la Reli, Mgodi wa Kiwira, Meremeta na uuzaji wa nyumba za Serikali na nyinginezo, ni miongoni mwa ufisadi uliojadiliwa na unaoendelea kujadiliwa. Kilichojitokeza na sasa ni dhahiri ni chama tawala CCM na serikali yake kuyumba. Aidha, kumejitokeza malumbano kati ya Serikali, Bunge na Mahakama ambayo yalilitikisa taifa. Chanzo cha mgogoro huu kama nilivyopata kutoa maoni yangu kwenye vikao vya CCM, na kwa mtazamo wangu wa hadi sasa ni sababu zifuatazo.Kama nilivyokwisha elezea mara kadhaa, chimbuko au kiini ni wafanyabiashara wala rushwa kujiunga kwa wingi CCM kama wafadhili na baadaye kupata nafasi za uongozi ndani ya chama na hatimaye serikalini.Hali hii ilianza kujitokeza kwa nguvu mwaka 1995 kwa wafanyabiashara wengi kujiunga na CCM na baadaye kugombea ubunge na hatimaye kupata nafasi za uongozi. Baada ya wafanyabiashara wala rushwa kuingia kwenye serikali, ndipo ubadhirifu mkubwa au ufisadi ulianza kutokea na kushamiri, mfano wizi wa EPA, Meremeta, kuingiwa mikataba mibovu kwenye sekta ya madini, uuzaji wa mashirika ya umma, ununuzi wa ndege ya rais, na rada. Matajiri wala rushwa wamepata sauti kwenye CCM na itikadi yake imefifia. CCM ilitetea wanyonge, wakulima na wafanyakazi, kwa sasa inatetea wafanyabiashara. Pengo kati ya matajiri na maskini limekuwa kubwa sana.Wananchi wanyonge hawatetewi na chama hiki tena. Kumejitokeza uhasama kwa wanachama, uhasama kati ya wabunge wa CCM na viongozi wa CCM ngazi za wilaya na mikoa ni kielelezo cha chama kuyumba. Kwa hali hiyo, Mwenyekiti wa chama aliunda tume iliyokuwa chini ya Rais wa pili, Ali Hassan Mwinyi. Tume hiyo maarufu kama “Tume ya Mzee Mwinyi” ilikuwa imepewa jukumu la kutafuta chanzo cha kuwapo chuki baina ya wabunge wa CCM na kati yao na mawaziri, kisha ishauri njia za kumaliza tofauti hizo na kukirudisha chama kwenye umoja.Mtakumbuka mwaka 2008 hadi 2010 ndani ya CCM kulikuwa na kuchukiana kwa wanachama, viongozi na wabunge.Hali ya kuchukiana ilikuwa imeelezwa na Mwenyekiti wa chama taifa kwamba, uhasama kati ya wanachama wa CCM ulifikia kiasi cha kuogopana hata wakati wakiwa wanakunywa vinywaji mahali; mmoja akitoka akirudi kama aliacha chupa ya bia nusu au soda anaogopa kuinywa. Hakuwaamini wanachama wenzake. Wakati huohuo viongozi walikuwa wakihubiri umoja. Unafiki mtupu! Hali hiyo ilifanana kwa kiasi fulani na kile kilichowahi kutokea wakati fulani huko nchini India ambako ilifikia hatua ya watu India kusema, “if you enter a room and in that room you find a cobra and an Indian, kill first the Indian because you may be able to compromise with the cobra”. Na kama alivyosema Mandela chuki hufunga akili na huzuia ubunifu wa aina yoyote. Hivyo niliona ndani ya CCM kuchukiana kulishamiri nikaanza kutafakari kuondoka. Ili kutafuta suluhu ya hali ilivyokuwa ndani ya CCM, katika kikao cha Tume ya Mwinyi, kikao ambacho wabunge wa CCM walialikwa kutoa maoni yao juu ya hali hiyo, nilipata nafasi ya kutoa maoni na mtazamo wangu. Nilianza kwa kueleza kutoridhishwa na mwenyekiti kuteua Kamati ya Mzee Mwinyi. Nilieleza utamaduni mbovu wa viongozi wa nchi nyingi za Kiafrika kupenda kuunda kamati na tume kwa sababu tu ya kuogopa kuchukua maamuzi magumu katika kutatua matatizo yaliyo dhahiri. Kwanini uunde kamati wakati suala lenyewe linaeleweka....? Kwanini usifanye maamuzi moja kwa moja....? Nilieleza mfano wa baba mwenye nyumba ambaye anaamua kuunda kamati ya kuua nyoka aliyeingia chumbani kwake au anateua tume ya kuandaa utaratibu wa kumuua nyoka. Si sahihi hata kidogo. Kufanya hivyo ni woga, ni vyema kuchukua hatua ya kumuua nyoka.
Katika mjadala huo pia nilieleza bayana bila kutafuna maneno kwamba CCM itilie mkazo itikadi yake, na isimamie vita dhidi ya ufisadi kwa nguvu zote, kwani katiba yake inaonyesha kuwa kipaumbele chake ni kupiga vita rushwa, dhuluma na ufisadi wote. Katika kikao hicho viongozi walininunia. Kilikuwa kikao kizito cha usuluhishi cha Tume ya Mzee Mwinyi. Katika kikao hicho nilisisitiza nikisema; “wale wanaotafuna maneno juu ya ufisadi, wapishe, waondoke kwani wamepingana na Katiba ya CCM. Au Katiba ya CCM ibadilishwe na iseme wazi kwamba CCM haipigi vita rushwa, dhuluma na haipingi watu wachache kumiliki utajiri wa nchi. Likifanyika hili wapo watakaoondoka”- (hapo ukumbi uliguna). Pia nilisisitiza kwamba, wale waliotuhumiwa na kuwajibika serikalini kwa kuhusika na kashfa ya Richmond ni vyema pia kwenye chama wawajibike akiwemo rais mstaafu Benjamin Mkapa. Bila hawa kuwajibika kwenye chama, kitaendelea kuwa na harufu ya ufisadi. Kulisema hili ilikuwa ni sawa na kuukumbatia mbuyu, ilikuwa kazi ngumu. Kwa kawaida kuuzunguka mbuyu ni rahisi.
Wabunge wengi walinizomea, lakini baadaye ilithibitika kwamba walinunuliwa ili wazomee, wagune na kufanya dhihaka!.
Baadhi ya mambo yaliyoigawa Serikali ya CCM ni kuhusu kauli kwamba Mkapa aachwe apumzike. Kauli hiyo iliyotoka kwa viongozi wa CCM na ni kauli tete na imewagawa wananchi kama ifuatavyo. Wapo wanaoona kwamba Mkapa alifanya mambo mengi mazuri katika uongozi wake. Wapo wanaoona kwamba urais ni taasisi, hivyo Mkapa kuwajibishwa si sahihi. Wapo wanaoona katika utawala wa Mkapa ubadhirifu ulikuwa mkubwa, hasa ule wa kutumia vibaya madaraka, hivyo awajibishwe. Maoni yangu juu ya suala hili ni kwamba, ni kweli katika utawala wa Mkapa yapo mazuri yaliyofanywa na upo ubadhirifu uliofanywa wa kutumia vibaya madaraka mfano kununua mgodi wa Kiwira katika utaratibu ambao ulikiuka maadili ya uongozi.
Ni vyema basi tuanze kujenga taifa lenye wananchi wenye kufuata maadili. Mkapa kwa niaba ya viongozi wengine wa utawala wake awaombe radhi Watanzania, hili litawafanya Watanzania wamwelewe na atapata heshima sana.
Pili kusema Mkapa apumzike ni msafi wapo baadhi tulioona hili si sawa. Kama kwenye uongozi wake kulitokea yafuatayo;
• Ufisadi wa EPA
• Uuzaji holela wa mashirika ya umma kama iliyokuwa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) na Shirika la Reli (TRC).
• Serikali yake kuingia mikataba mibovu kwenye sekta ya madini.
• Uuzaji wa nyumba za serikali.
• Ununuaji wa Mgodi wa Kiwira
• Ufisadi wa Meremeta
• Ununuzi wa rada na ndege ya rais
Je, aliyesimamia haya aitwe msafi? Hapana, huko ni kulindana. Tukiendelea kusema Mkapa ni msafi au kiongozi bora tutawachanganya wananchi, maana watashindwa kupambanua uadilifu ni upi na ufisadi ni upi – huu ni ukweli uliofichwa, lakini ni ngumu sana kuendelea kuuficha. Kwa mtazamo wangu ni vyema iwekwe bayana na Serikali ya CCM kwamba Mkapa alitumia madaraka vibaya na ashauriwe kujitokeza kuwaeleza Watanzania yeye mwenyewe. Ikitokea rais mchaguliwa akazidisha ujasiri na vituko vya ufisadi atawajibishwa vipi wakati hili la Mkapa litakuwa limeweka utaratibu kwamba rais akimaliza awamu yake anaachwa apumzike tu bila kujali rekodi yake ya utendaji? Je, na wengine walio mahakamani sasa pia waachwe wapumzike?
Tukumbuke wapo wananchi wengi wanateseka kutokana na maamuzi mabaya ambayo yalifanywa bila kujali maslahi ya nchi. Wananchi wengi wapo kwenye lindi kubwa la umaskini kutokana na utumiaji mbaya wa madaraka. Wananchi wengi wanaumia kutokana na mikataba mibovu na uuzaji wa mashirika ya umma. Je, ni haki Watanzania hao wateseke, lakini waliokiuka maadili wapumzike? Hapana. Tukumbuke pia madaraka wanayokabidhiwa watawala na viongozi ni dhamana kubwa inayotakiwa kuheshimiwa hata kuogopewa. Hivyo, tuweke utaratibu utakaofanya yeyote anayepewa madaraka aheshimu na kuiogopa dhamana hiyo, vinginevyo tutawachanganya wananchi kwa falsafa ya kusema apumzike na watashindwa kupambanua uadilifu na ufisadi, matokeo yake maadili nchini yataendelea kumomonyoka na nchi itaoza. Hata hivyo, ushauri huu nilioutoa ndani na nje ya Bunge kuhusu Mkapa kuwajibika mwenyewe au kuwajibishwa na Serikali, bado umekuwa mgumu kutekelezwa na hakuna dalili kama wenye mamlaka watautekeleza, lakini yote hii ni kwa sababu CCM inayumba.
Imeshindwa kusimamia misingi na maadili yaliyopo kwenye katiba na kanuni zake badala yake wameamua kulindana huku taifa likiumia.
Jambo jingine nililolisisitiza ni kutambua kwamba uongozi ni dhamana, nikinukuu ule msemo wa Kiingereza “A friend in power is a friend lost” unaomaanisha, rafiki aliyepata dhamana kubwa ya madaraka, anakoma kuwa rafiki. Niliwashauri wale waliokuwa marafiki wa wanamtandao wa rais wamwache awatumikie Watanzania wote, si rais wa wanamtandao au rais wa wanafamilia – ni rais wa wote. Huo ndiyo ulikuwa sehemu ya mchango wangu katika kikao hicho cha chama wakati bado nikiwa mwanachama wa CCM. Kikao hiki hakikuwa chepesi.
Baada ya kikao hicho, hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa na badala yake nikaanza kuandamwa ili nifukuzwe CCM.
Taerehe 30 Machi, 2010, nilitangaza kujiondoa CCM. Nilikatiwa mawasiliano ya simu. Nilifuatiliwa na vyombo vya usalama kama mhalifu na haini. Hali ya utendaji kazi ndani ya vyombo mbalimbali ilinisaidia kupata taarifa za mara kwa mara za jinsi nilivyokuwa nafuatiliwa. Nilipohama CCM, tarehe 30 Machi, 2010, nilikuwa nimebakiza mikutano miwili tu ya Bunge ili kustahili kulipwa haki zote. Nilijua nikitoka ningepoteza baadhi ya mafao, lakini naomba nieleweke kuwa nilikuwa nimechoshwa na CCM. Bila kuondoka wakati ule, ulikuwepo uwezekano wa roho yangu kutengana na mwili kwa maumivu niliyokuwa nayapata.Nimetambua sasa kwamba wakati mwingine tuwe tayari kujitolea kufanya mambo au kuchukua maamuzi ambayo yataleta mafanikio, si kwetu sisi tu kwa wakati huu, bali yatalete mafanikio baadaye kwa faida ya watu wengine. Watu wanaoweza kufanya hivyo ndio watakaoleta mabadiliko yanayopasa, watu wa aina hiyo ni wachache sana.
Nakubaliana pia na kauli ya Budha: “Usiamini jambo lolote kwa vile tu mtu mwenye hekima amelisema. Usiamini jambo lolote kwa vile tu jambo hilo linakubalika na kila mtu. Usiamini jambo lolote tu kwa vile limeandikwa katika vitabu vya kale. “Usiamini jambo lolote tu kwa vile linasemekana ni takatifu. Amini jambo ambalo wewe mwenyewe umelipima na kukubalika kuwa kweli”. Pamoja na kushauriana na marafiki zangu, kuondoka kwangu CCM msingi wake ni huu, niliamini mimi mwenyewe ukweli kwamba CCM imefikia ukomo na haitawasaidia Watanzania tena. Nimetambua pia kuwa mtu akikubali kupoteza kila kitu kwa ajili ya jamii, jamii hiyo itamheshimu. Mwalimu Nyerere alipojiuzulu uwaziri mkuu, aliheshimika zaidi. Ali Hassan Mwinyi alipojiuzulu kwa dhati kama Waziri wa Mambo ya Ndani, aliheshimika zaidi na akaja akawa rais wa nchi. Wapo wanaojiuzulu vyeo kwa hila, kisha, kwa mlango wa nyuma hununua watu wawasafishe.
Hawasafishiki kwa njia hiyo. Ni kanuni ya dunia hii na ijayo kwamba kabla ya utukufu ni lazima unyenyekevu utangulie. Bila unyenyekevu, hakuna utukufu wa kweli. Wanaohangaika kujisafisha kwa kuwanunua watu na kutumia fedha nyingi wanapoteza fedha zao bure, kwani wananchi wanajua na wanayakumbuka matendo maovu waliyoyatenda kwa jamii. Kama ulitenda maovu, njia pekee ya jamii kukukubali tena ni kujutia uovu wako na wala si kujisafishwa kwa udanganyifu, kwani kufanya hivyo huzidisha hasira ya jamii. Ninapohitimisha makala hii napenda kusisitiza: Heri wenye njaa na kiu ya haki, maana hao watashibishwa. Mabadiliko yanawezekana,tukiamini. Pasipo imani,hakuna kinachowezekana. Ukiwa na imani, hakuna lisilowezekana.
Na pasipo mashauri, taifa huanguka, bali kwa wingi wa washauri, huja wokovu; Mema hushinda mabaya; Ukweli hushinda uongo na Upendo hushinda uovu; Harakati zetu zitafanikiwa na TUTASHINDA.
Mwandishi wa Makala hii ni Fred Mpendazoe ( 0762 92 6556 ). Alikuwa Mbunge wa Jimbo la Kishapu kupitia CCM kuanzia November 2005 hadi Machi 2010 alipojiuzulu kutokana na kutoridhishwa na mwenendo ndani ya CCM.

KILA MZANZIBARI ATAULIZWA SIKU YA KIYAMA NA MWENYEZI MUNGU ULIPOSIKIA WAZANZIBARI WENZIO WANADHALILISHWA NA KULAWITIWA NA HAWA JE ULIFANYA NINI TAFUTA JIBU LAKO MAPEMA KWA SIKU HIYO YA KIYAMA SIKU AMBAYO MALI NA WATOTO WAKO WALA CHEO CHAKO HAVITAKUFAA SIKU HIYO.

No comments:

Post a Comment