Sunday, May 22, 2016

MAELEZO YA NAIBU KATIBU MKUU WA CHAMA CHA WANANCHI CUF MHE. NASSOR AHMED MAZRUI. TAARIFA YA UVUNJWAJI WA HAKI ZA BINADAMU ZANZIBAR 2015/2016




MAELEZO YA NAIBU KATIBU MKUU WA CHAMA CHA WANANCHI (CUF), MHE. NASSOR AHMED MAZRUI, KWENYE MKUTANO MAALUM NA WAANDISHI WA HABARI KWA AJILI YA UZINDUZI WA TAARIFA YA UVUNJWAJI WA HAKI ZA BINADAMU ZANZIBAR 2015/2016
LAMADA HOTEL, DAR ES SALAAM – 22 MEI, 2016
UTANGULIZI:
Kipindi cha kuelekea Uchaguzi Mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015 kilishuhudia kurudi upya kwa matukio ya uvunjwaji wa haki za binadamu na uhalifu dhidi ya binadamu na utu wao kwa kiwango kikubwa visiwani Zanzibar.
Matukio haya yalishika kasi wakati wa uandikishaji wa wapiga kura wapya katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura katika miezi ya Aprili hadi Juni 2015, yakaendelezwa wakati wa kampeni za uchaguzi mkuu na kuibuka tena kwa kiwango cha kutisha baada ya kile kilichoitwa tangazo la Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar, Jecha Salim Jecha, la kufuta uchaguzi mkuu wa tarehe 25 Oktoba, 2015 na kuendelea hadi sasa.
Uvunjwaji huo wa haki za binadamu ulihusisha:
1. Kuibuka kwa makundi ya maharamia ambao wananchi wamekuwa wakiwaita MAZOMBI ambao hufunika nyuso zao na huku wakibeba silaha za moto na silaha za kienyeji na wakiwa ndani ya gari zenye namba za Vikosi Maalum vya SMZ wamekuwa wakipiga, kuwaibia mali zao, kuwajeruhi na hata kuwakata sehemu za miili yao wananchi wasio na hatia katika maeneo mbali mbali ya visiwa vya Unguja na Pemba.
2. Kuvamiwa kwa misafara ya wanachama na wafuasi wa CUF waliokuwa wakirudi kutoka kwenye mikutano ya kampeni na kupigwa na watu waliokuwa wamevalia sare za CCM na huku wengine wakiwa wamejifunika nyuso zao.
3. Kuwashambulia wananchi wasio na hatia kwa kutumia risasi za moto kulikofanywa na Polisi na Vikosi vya SMZ ambako kumepelekea watu kadhaa kujeruhiwa vibaya.
4. Matukio ya ubakaji dhidi ya wanawake.
5. Unyanyasaji wa kijinsia dhidi ya mahabusu wanawake waliokuwa katika mikono ya Polisi.
6. Kutekwa watu na kuwatesa wanapokuwa katika mikono ya watekaji.
7. Kukamatwa ovyo na kuwekwa ndani kwa watu wasipoungua 90 wakiwemo viongozi waandamizi wa CUF bila ya kuwafungulia mashtaka Mahkamani kinyume na Sheria za Mwenendo wa Makosa ya Jinai Zanzibar.
8. Kuwatesa na kuwaadhibu wanachama na wafuasi wa CUF waliokuwa chini ya mikono ya Polisi ambao hawakufikishwa Mahkamani huku wakilazimishwa kukiri kutenda makosa ambayo hawakuyatenda.
9. Kuchoma na kuvunja ofisi za matawi na majimbo ya CUF pamoja na baraza zinazotumiwa na wanachama na wafuasi wa CUF kwa kukutana na kubadilishana mawazo.
10. Kuchoma nyumba za wanachama na wafuasi wa CUF katika vijiji mbali mbali Unguja na Pemba.
11. Kuharibu miundombinu ya maji na huduma nyengine muhimu za jamii katika maeneo ambayo yana wafuasi wengi wa CUF.
12. Kuvamiwa kwa kituo cha redio binafsi na kuwatishia maisha waandishi wanaotangaza vipindi visivyowaridhisha watawala na kuchoma moto kituo kimoja cha redio binafsi.
13. Kutoa hotuba za kuchochea fujo, ubaguzi na vitisho kulikofanywa na wanasiasa waandamizi wa CCM ikiwemo kuruhusu mabango yanayochochea ubaguzi na chuki kwa jamii nzima ya watu walioitwa “MACHOTARA”.
14. Redio na Televisheni za Serikali kutayarisha na kurusha vipindi vinavyochochea shari, fujo na ubaguzi katika jamii.
15. Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia ofisi zake za MASKANI YA KISONGE kuweka ubao maalum unaoitwa “SAUTI YA KISONGE” unaotumiwa kuandika na kusambaza ujumbe wenye kuchochea ubaguzi, fujo na ghasia dhidi ya watu wa jamii fulani hasa Wapemba na wanachama na wafuasi wa CUF.
16. Kuendesha kampeni za vitisho na kuleta hali ya taharuki na hofu kwa kupitisha askari wakiwa na silaha nzito nzito pamoja na magari ya kivita katika maeneo yenye makaazi ya raia visiwani Unguja na Pemba huku wakiimba nyimbo za ubaguzi kwa mfano kusema “HATUWATAKI MACHOTARA”.
UZINDUZI WA TAARIFA YA UVUNJWAJI WA ZA HAKI ZA BINADAMU:
Chama Cha Wananchi (CUF) kimeweka kumbukumbu za matukio yote haya na kimetayarisha Taarifa ya Uvunjwaji wa Haki za Binadamu ambayo leo hii tutaizindua hapa.
Nimuombe Naibu Mkurugenzi wa Haki za Binadamu na Sheria, Mhe. Pavu Juma Abdalla, awasilishe kwenu muhtasari huo wa Taarifa hiyo. Mwisho wa mkutano huu tutawapatia nakala za Taarifa hiyo kila mmoja.
Baada ya kupokea Muhatasari huo, niwaeleze kwamba matukio haya na mengine yamechafua sana taswira na jina la Tanzania katika jumuiya ya kimataifa.
Katika mapitio ya kila mwaka ya haki za binadamu nchini Tanzania (Universal Periodic Review) yanayofanywa na Umoja wa Mataifa kupitia United Nations Human Rights Council ambayo yamefanyika mjini Geneva, Uswisi tarehe 2 – 13 Mei, 2016 yaani mwezi huu, mataifa kadhaa duniani yaliibana Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusiana na matukio haya na mengine.
Kiongozi wa ujumbe wa Tanzania katika mapitio hayo, Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome, alipata wakati mgumu kujibu hoja hizi.
Rekodi zote za mkutano huo zinapatikana katika mtandao. Miongoni mwa maazimio yaliyotolewa kwa Tanzania kutoka mataifa mbali mbali wanachama wa Umoja wa Mataifa ni pamoja na haya yafuatayo (na nayanukuu kwa Kiingereza kama yalivyoripotiwa kwenye mtandaohttp://www.upr-info.org/database/index):
* Ensure that police officers having committed acts of torture of illtreatment be prosecuted and punished appropriately
- Recommended by Belgium
- Response: Accepted
* Take adequate measures to protect its population from violence committed by the security forces and establish an independent mechanism for the investigation of complaints regarding abuses carried out by law enforcement officials
- Recommended by Denmark
- Response: Accepted
* Establish an independent body for investigating complaints about the actions of law enforcement officials
- Recommended by United Kingdom
- Response: Accepted
* Provide all victims of violence against women an unhindered access to justice and ensure that all perpetrators are brought to justice in accordance with international standards
- Recommended by Slovakia
- Response: Accepted
Improve the efficiency of the justice system by streamlining and simplifying judicial procedures including introducing a case management system that tracks individual cases from filing to disposition and limits the amount of time each case can be held at each stage
- Recommended by Canada
- Response: Accepted
* Vigorously prosecute security force personnel who violate the law
- Recommended by United States
Response: Accepted
* Ensure all security forces are subject to strict control of civilian authorities
- Recommended by United States
- Response: Accepted
* Guaranteeing the freedom of expression, association and assembly by allowing human rights defenders, political opponents and journalists to express freely their views in line with international human rights law
- Recommemded by Netherlands
- Response: Accepted
* Work with the media and other stakeholders to ensure that all organs of the State understand and appreciate the constitutional guarantees of freedoms of press and assembly
- Recommended by United States
- Response: Accepted
* Step up its efforts to protect women and girls from sexual violence
- Recommended by Norway
- Response: Accepted
* Work to abolish laws that restricts freedom of expression, information and freedom of media, and establish laws that will guarantee these rights in line with international human rights standards
Recommended by Sweden
Response: Accepted
* Respect the right to assembly throughout the process of reviewing the Constitution
- Recommeded by Norway
- Status: Accepted
Kama inavyoonekana maazimio yaliyoorodheshwa hapa ambayo pia yanaonyesha nchi gani iliyatoa yalikubaliwa na Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia Katibu Mkuu wa Wizara ya Katiba na Sheria Prof. Sifuni Mchome. Yote tuliyoyanukuu hapa yameripotiwa kwamba ni “ACCEPTED” yaani yamekubaliwa.
Hata hivyo, wakati maazimio haya na kukubaliwa kwake kukiwa ndani ya mwezi huu huu, bado tumeshuhudia uvunjwaji wake ukiwa unaendelea.
Matukio ya watu kuvamiwa katika maeneo yao na kupigwa ovyo yameshamiri upya wiki hii hususan kisiwani Pemba hasa baada ya ziara ya Katibu Mkuu wa CUF na mshindi wa nafasi ya Urais wa Zanzibar katika uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 25 Oktoba, 2015, Maalim Seif Sharif Hamad ambayo ilikuwa ya mafanikio makubwa.
Tunazo taarifa kwamba kuna wanasiasa wameliagiza Jeshi la Polisi kuandaa mashtaka kwa ajili ya kumshtaki Maalim Seif kwamba eti alipokuwa Pemba alifanya maandamano bila ya kibali wakati hakukuwa na maandamano yoyote.
Tunazo taarifa pia kwamba kuna njama za kuwakamata tena viongozi mashuhuri wa CUF na hasa Mhe. Mansoor Yussuf Himid na Mhe. Mohamed Ahmed Sultan (maarufu kwa jina la Eddy Riyami) na kuwaleta katika magereza ya Tanzania Bara kwa lengo la kuwanyamazisha Wazanzibari ili wasipaze sauti zao kupinga utawala wa kidikteta uliowekwa madarakani kwa nguvu za dola kinyume na matakwa ya kidemokrasia ya wananchi wa Zanzibar.
HATUA TUTAKAZOCHUKUA:
Baada ya hatua ya leo ya uzinduzi wa Taarifa hii, Chama Cha Wananchi (CUF) kimejiandaa kuchukua hatua zifuatazo:
1. Kumuandikia rasmi Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dk. John Pombe Magufuli, na kumkabidhi nakala ya Taarifa hii ili ajue kinachofanyika nchini na hasa akiwa Amiri Jeshi Mkuu.
2. Kuiwasilisha Taarifa hii pamoja na vielelezo vyote katika jumuiya, taasisi na mashirika ya kimataifa yanayotetea haki za binadamu ulimwenguni kwa hatua zao.
3. Kuiwasilisha Taarifa hii pamoja na vielelezo vyote katika Tume ya Haki za Binadamu na Utawala Bora hapa nchini ambayo hata katika mkutano wa Geneva ilitambuliwa uwepo wake, Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHRC), Kituo cha Huduma za Sheria Zanzibar (ZLSC) pamoja na taasisi nyengine zinazoshughulikia masuala ya haki za binadamu hapa nchini.
4. Kufungua kesi katika Mahkama Kuu ya Tanzania dhidi ya Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi na Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) kuhusiana na matendo yanayohusisha Jeshi la Polisi visiwani Zanzibar. Tayari, tokea mwezi uliopita mwanasheria wetu ameshawasilisha taarifa rasmi kwa Waziri na IGP kuhusu nia hiyo kama sharia zetu zinavyotaka ikiwa ni hatua ya kwanza katika kufungua kesi hiyo.
5. Kuendelea na hatua ya kukamilisha taratibu zitakazoiwezesha Mahkama ya Kimataifa ya Uhalifu (International Criminal Court – ICC) kuanzisha uchunguzi dhidi ya watu wenye dhamana mbali mbali ambao wamehusika kuchochea, kutoa au kusimamia maagizo yaliyopelekea makosa dhidi ya ubinadamu na makosa yanayoilenga jamii fulani ya watu. Jopo la wanasheria wetu limeshaanza kazi hiyo wakiwemo wanasheria wa kimataifa waliobobea katika kesi za ICC. Tayari kampuni moja ya wanasheria tuliyoipa kazi hii imeshawaandikia rasmi ICC kuhusiana na suala hili.
MWISHO:
Tunawapongeza na kuwashukuru wananchi wote wa Zanzibar wanaokandamizwa na kuteswa kwa sababu tu ya kutetea utu wao na haki zao kwa moyo wao wa ujasiri, ushapavu na uvumilivu katika kukabiliana na ukandamizaji huu na mateso yanayowakuta.
Tunawahakikishia kwamba Chama Cha Wananchi (CUF) ambacho wamekiamini na kukipa ridhaa yao kitaendelea kuwa pamoja nao na kutetea haki zao ikiwemo haki yao ya kuheshimiwa chaguo lao la kiongozi yupi na chama gani kiwaongoze. Sisi kama viongozi wao hatuna wasiwasi kwamba kwa mashirikiano ya pamoja HAKI ITASIMAMA NA UTU UTASHINDA.
Ahsanteni kwa kunisikiliza.

No comments:

Post a Comment