Monday, May 28, 2012

MATEMBEZI YA AMANI KUDAI NCHI YA ZANZIBAR KUWA HURU YAFANYIKA NCHINI ZANZIBAR


WAZENJI WAKIANDAMANA KWA AMANI KUDAI NCHI YETU YA ZANZIBAR

WAKINA MAMA NA DADA PIA WAKIANDAMANA KUDAI NCHI YETU YA ZANZIBAR
Maelfu wa wazanzibari wakiongozwa na Taasisi za Kiislamu na Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI) wakifanya matembezi ya amani katika barabara za Zanzibar na kupeleka ujumbe wao kwa viongozi wa serikali za Zanzibar na ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania pamoja na Umoja wa Mataifa wakitaka Zanzibar huru ambapo baadhi ya watembeaji hao wakiongoza na Kiongozi wa Jumuiya hizo, Sheikh Farid Hadi Ahmed na viongozi wengine
Maelfu ya wazanzibari leo wamefanya maandamano amani kuishindikiza Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuitisha kura ya maoni juu ya Muungano na kupeleka ujumbe kwa Umoja wa Mataifa wa kutaka Zanzibar kujitenga kama ilivyofanya Sudan ya Kusini.
Wazanzibari hao wakiongozwa na Sheikh Farid Hadi Ahmed walitembea kutoka viwanja vya Lumumba na kupitia barabara ya Kinazini, Mpigaduri, Michenzani Maskani ya CCM Kisonge, kwa Biziredi na kurudi tena viwanja vya Lumumba.
Maandamano hayo walioyaita matembezi ya amani yalifanyika na kuhudhuriwa na maelfu ya wazanzibari ambapo awali kuliandaliwa kongamano kubwa lililoandaliwa na Taasisi za Kiislamu kwa kushirikiana na Jumuiya ya Uamsho na Mihadhara ya Kiislamu Zanzibar (JUMIKI) kwa lengo la kuzungumzia mfumo wa elimu Zanzibar.
Akizungumza na maelfu ya wazanzibari kabla ya kuanza maandamano hayo yaliitwa ni matembezi ya amani, Sheikh Farid alisema wazanzibari wana haki kama walivyokuwa na haki wananchi wengine ulimwenguni kote kudai haki yao ndani ya nchi yao.
“Sisi wazanzibari kama wananchi wengine wowote duniani tuna haki ya kikatiba kudai nchi yetu kama walivyodai Sudan ya Kusini, mbona Sudan ya wameweza kujitenda na kupata nchi yao kwa nini sisi kama wazanzibari tusikubaliwe kudai nchi yetu sasa sisi tunampelekea salam katibu mkuu wa umoja wa mataifa kumwambia kuwa wazanzibari sasa wanataka nchi yao” alisisitiza Sheikh Farid huku akiungwa mkono kwa mamia hao kuinua mikono na kusema ndiooooo.
Awali Sheikh Farid alisema salamu hizo anataka zimfikie Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Ban Kin moon ambaye kwamba wazanzibari wamechoshwa na kuwepo ndani ya Muungano ambao umedumu kwa miaka 48 lakini bado ukiwa na kero nyingi na malalamiko ambayo yanaonekana utatuzi wake ni mdogo na usiowezekana ambapo alisema Muungano wa Tanganyika na Zanzibar hauna manufaa yena na wazanzibari.
Katika kuonesha kwamba hawataki tume ya katiba ije kuchukua ya maoni ya katiba mpya Sheikh Farid alisema wanataka kwanza kuamuliwe suala la Muungano kabla ya jambo lolote na kuahidi kwamba wataendelea kufanya makongamano, mihadhara na maandamano kwa kadiri wawezavyo hadi hapo serikali itakaposikia kilio hicho.
“Ujumbe huu tunautoa kwa Ban Kin moon, na kwa ulimwengu mzima lakini pia tunataka rais wetu Dk Shein asikie kilio hiki na Rais Kikwete ambaye yeye ni mtetezi wa haki za binaadamu na pia ni mfuatiliaji wa nchi zinazovunja haki za binaadamu tunataka asikie kilio cha wazanzibari kuwa wanataka nchi yao” alisema.
Alisema juzi wamefanya maombi maalumu ya kumuombea Rais wa Zanzibar lengo likiwa ni kumjaaliwa kheri na awe na maamuzi sahihi juu ya wananchi wa Zanzibar sambamba na kuwaomba Makamu wa Kwanza na makamu wa Pili wa Zanzibar kusikia kilio cha wazanzibari wasiotaka Muungano.
“Tunamuomba Rais wetu Dk Shein, Makamu wa Kwanza Maalim Seif na Makamu wa Pili Balozi Seif kwamba sisi wazanzibari tunahitaji Zanzibar huru, tunahitaji heshima ya nchi yetu na tupo tayari kwa lolote kwa hivyo tunataka salamu hizi na ujumbe huu ukufikieni” alisema Sheikh Farid huku akiungwa mkono na maelfu waliohudhuria katika kongamano hilo ambalo awali liliandaliwa kwa lengo la kuzungumzia masuala la elimu na mfumo wake.
Akiendelea kutoa salamu hizo mara Sheikh Farid alisoma kifungu cha 16 cha katiba na kuwaleza wananchi kwamba haki ya kutembea ni haki ya kila mwananchi ambayo imeainishwa katika katiba na sheria za haki za binaadamu hivyo aliwageukiwa na kuwataka wasimame na kisha kumfuata yeye.
“Haki ya kutembea ni haki ya msingi kwa mujibu wa sheria na kifungu cha 16 kinatupa haki ya kutembea sasa mimi nataka kutembea jeee mpo tayari kutembea na mimi? Alihoji Sheikh huyo huku akijibiwa na umma mkubwa kwamba ndioooo”
Aliongeza kwamba “Tunaanza kutembea na tuone mtu atukamate tunakwenda njia ya kinazini, tunapita michenzani, tunapita barabara ya kwa biziredi na kisha tunarejea hapa hapa kuendelea na kongamano letu kwa amani kabisa mmesikia….akajibiwa ndiooooo”
baada ya kusema hivyo Sheikh Farid alitoa takbir na kuanza kukamatana mikono na viongozi wenzake na huku ummati mkubwa ukiwa umekamatana mikono nyuma na kuanza safari kwa pamoja na kutembea katika barabara ambazo walizitaja awali.
Waandamani hao walikamata mabango yenye maandishi mbali mbali ikiwemo hatutaki muungano, tunataka nchi yetu, zanzibar bila ya muungano inawezekana na wengine kadhalika huku wakitembea njiani na kupiga takbir ambapo walikuwa wakisema Mwenyeenzi Mungu Mkubwa, Mwenyeenzi Mungu Mkubwa sisi hatuna uwezo isipokuwa tunakutegemea wewe Mwenyeenzi Mungu.
Waandamanaji hao walianza kutembea kwa utaratibu maalumu huku magari yakizimama na kuwapisha bila ya kuwepo jeshi la polisi ambapo viongozi wa jumuiya hiyo na wananchi wengine waliongoza utaratibu huo na kutembea katika barabra kwa utaratibu mzuri hadi kumaliza maandamano yao waliyoyaita matembezi ya amani.
Awali akitoa mada katika kongamano hilo, Maalim Abdulhafidh Malelemba alisema sekta ya elimu imekuw aikidorora Zanzibar kutokana na kukandamizwa na mambo ya Muungano ambapo kila mwaka wanafunzi wanapofanya mitihani kufelishwa kwa makusudi huku idadi ya wanafunzi wanaokwenda katika vyuo vikuu wakiwa kidogo kutokana na kufelishwa katika mitihani ambapo husainiwa na baraza la mithani Tanzania (NECTA).
Wakizungumza katika nyakati tofauti katika kongamano hilo, baadhi ya walimu walisema kukosekana kwa baraza la mitihani Zanzibar kusimamia mitihani ya elimu ya juu ndio sababu ya wazanzibari kufelishwa kwa wingi na kushindwa kuingia katika vyuo vikuu kwa kuwa wanafunzi wengi wa Zanzibar hufelishwa.
Walimu hao walitoa ushahidi wa hivi karibuni wa kufelishwa wanafunzi wa kidatu cha nne ambapo walisema lile ni tukio la makusudia lililofanywa na baraza la mitihani ikiwa ni kuwadhoofishwa wanafunzi wa Zanzibar ili wasiendelee katika masomo kwa kuwafelisha

No comments:

Post a Comment