Thursday, July 18, 2013

WANAJESHI WA NCHI YA TANGANYIKA WALIOULIWA DARFUR MAITI ZAO ZINATARIJIWA KULETWA NA NDEGE YA U.N. JUMAA MOSI


Dar/mikoani. Wakati miili ya majeshi wa nchi ya Tanganyika waliouliwa na kikundi cha wapiganaji wa  Darfur ikitarajiwa kuletwa keshokutwa, ndugu, jamaa na marafiki wa marehemu wameanza kuwasili Dar es Salaam kwa ajili ya kuipokea maiti hizo.

Msemaji wa Mpango wa Kulinda Amani wa Umoja wa Mataifa na Afrika (UNAMID), kwenye Mji wa Darfur, Chris Cycmakick alisema jana kuwa miili hiyo ilikuwa ikiendelea kufanyiwa uchunguzi ambao unatarajiwa kukamilika leo.

“Hata kama uchunguzi ukikamilika kesho (leo), hatuwezi kusafirisha keshokutwa (kesho Ijumaa) kwa kuwa hapa Sudan ni kama siku ya mapumziko. Sasa utaratibu unafanyika kuisafirisha Jumamosi kwa ndege ya Umoja wa Mataifa,” alisema Cycmakick.

Wapiganaji hao saba waliouliwa na moja ya vikundi vya waasi walipokuwa wakijaribu kuyafuatilia magari yao yaliotekwa na wapiganaji  huko Darfur.

Uchunguzi, ulibaini kuwa wanajeshi hao wanatoka vikosi vya 42KJ Chabruma, Songea, 44KJ Mbeya, 36KJ Msangani, 92KJ Ngerengere, 94KJ Mwenge, Dar es Salaam, 41KJ Makuu ya Jeshi- Upanga, Dar es Salaam.
  
Majina ya wanajeshi saba wa nchi ya Tanganyika waliouliwa Darfur                             
 
1) Rodney Ndunguru
2) Koplo Oswald Chaula
3) Peter Werema
4) Mohamed Chukilizo
5) Mohamed Juma, Lugalo
6) Sajini Shaibu Othman
7) Christopher Msofe

Wazazi na wake wa Familia zawasili Dar

Wakati miili ya wapiganaji hao ikitarajiwa kuletwa juma mosi, tayari familia zao zimeshawasili Dar es Salaam kwa ajili ya kuwapokea marehemu hao kwa maziko katika maeneo yaliyopangwa na wengine wakisubiri katika mikoa yao.

Akizungumza na mwandishi wetu wa siri wa FREE ZANZIBAR PEOPLE FROM MKOLONI MWEUSI jana eneo la Mji Mpya, Songea, Mama wa marehemu, Rodney Ndunguru, Lucy alisema wanachosubiri ni kupokea mwili wa marehemu watakapoletewa na jeshi kutoka Dar es Salaam.

Alisema mwili wa mtoto wake huyo aliyekuwa Kambi ya 92KJ, Ngerengere mkoani Morogoro utasindikizwa na mke wa marehemu, Fatma Hajj Ammen ambaye  alikwenda nchini Zanzibar kujifungua mtoto ambaye sasa ana miezi minne.Mama huyo alisema kuwa mwanawe huyo kifungua mimba na aliyekuwa katika kikosi cha makomandoo, atazikwa alikolala baba yake, eneo la Myangayanga, Songea.

Naye Maria Chaula, mke wa Koplo Oswald Chaula aliyekuwa Kikosi cha Mizinga katika Kambi ya Chabruma, aliondoka jana alfajiri kwenda Dar es Salaam kupokea mwili wa marehemu mume wake wakati watoto wake wanne wakitangulia Kijiji cha Mtitu Wilaya Kilolo, Iringa kwa taratibu nyingine za mazishi.

Mama wa marehemu Chaula, Zaina Mpagama, akiwa kijijini Mtitu, alisema mwanajeshi huyo ambaye ni mtoto wake wa sita na ni pekee wa kiume, ameacha pengo lisilozibika... “Baba, nimepata pigo, mwanangu pekee wa kiume jamani...,” alisema huku akilia kwa uchungu.

Mjini Mbeya, huzuni na simanzi zimetawaka katika Kambi ya 44KJ Mbalizi baada ya taarifa za kifo cha mwanajeshi wa miguu, Peter Werema. taarifa zinasema taratibu za mazishi na mahali atakakozikwa marehemu huyo zitafanyika mara baada ya mwili wake kuwasili.
Hata hivyo, taarifa zilizopatikana jana zilieleza kuwa marehemu ambaye ni mara yake ya pili kwenda Sudan ni mwenyeji wa Mkoa wa Mara na huenda akasafirishwa kwenda huko kwa mazishi.

Nayo familia ya marehemu Mohamed Chukilizo aliyekuwa Kambi ya Majimaji, 41KJ Nachingwea iliwasili Dar es Salaam jana kwa basi tayari kupokea mwili wa marehemu mpendwa wao.

Mtoto wa marehemu, Amina Mohamed anayesoma kidato cha nne Sekondari ya Nachingwea alisema jana kuwa anasikitika kumpoteza baba yake lakini anaamini kuwa ni mipango ya Mungu.

Amina alikuwa akisoma Nachingwea wakati mama yake yuko Dar es Salaam. Marehemu ambaye ni mwenyeji wa Mkoa wa Kigoma, huenda akasafirishwa kwenda mkoani humo kwa maziko.

Msiba mwingine uko nyumbani kwa kaka wa marehemu, Mohamed Juma, Lugalo Area J.  Hata hivyo, hali ilikuwa tofauti kwani hakukuwa na watu kwa kile kilichoelezwa kuwa mke wa marehemu tayari ametangulia Zanzibar ambako mwili wa mpiganaji huyo utapelekwa kwa maziko.
Habari zilizopatikana jana zilisema marehemu Juma ambaye alikuwa mkazi wa Dar es Salaam, mwili wake utasafirishwa kwenda Zanzibar baada ya shughuli ya kuaga miili hiyo Makao Makuu ya Jeshi, Upanga Dar es Salaam.

Mpiganaji mwingine ni Sajini Shaibu Othman kutoka Makao Makuu ya Jeshi, MMJ, ambaye familia yake inaendelea na utaratibu wa maziko nyumbani kwake, Kigamboni, Dar es Salaam.

Marehemu huyo aliyekuwa mwanajeshi wa miguu, ameacha mjane na watoto wawili. Mpiganaji huyo kama alivyo, Mohamed Juma wanatarajiwa kusafirishwa kwenda Zanzibar kwa maziko.

Mke wa mpiganaji, Christopher Msofe kutoka Kambi ya Jeshi Msangani, Pwani, Amina Juma akiwa nyumbani kwake Visiga alisema: “Bado tunapanga utaratibu wa kupokea mwili, lakini maziko yatakuwa Kange, Tanga.”

Msofe aliyekuwa mwanajeshi wa kikosi cha ardhini aliyehamia kambini hapo akitokea Moshi Kilimanjaro, hakubahatika kupata mtoto.

Wapiganaji saba waliouliwa na wengine 19 walijeruhiwa Jumamosi iliyopita na ilielezwa kuwa mauaji hayo yalisababishwa na wanajeshi hao kufuatilia magari yao yaliyokuwa yametekwa na kundi mojawapo la waasi.
Mmoja kati ya majeruhi walionusurika na kifo hicho amehamishwa kutoka Hospitali ya Nyala na kupelekwa Khartoum kwa matibabu zaidi.
                               

No comments:

Post a Comment