Saturday, June 18, 2011

MAALIM SEIF SHARIFF HAMAD IZINDUWA MADRASAT KADIRIA

mzalendo_mh Makamu wa kwanza akifunguwa madrassa
Salma Said,
Makamo wa kwanza wa Rais nchini Zanzibar, Maalim Seif Shariff Hamad amewataka walimu na wazee wa kijiji cha tomondo kushirikiana katika kuiendesha madrasa Kadiria Imman ili kuhakikisha vijana wao wanapata elimu bora yenye kufuata maadili ya dini ya kiislam kwa kufuata maelekezo ya vitabu vya Quraan na hadithi za Mtume Muhammad (SAW).
Amesema chuo kina jukumu kubwa la kuwafundisha wanafunzi elimu ambayo itawasaidia maisha ya dunia na akhera kwa kupitiya vitabu mbali mbali na kwa kusoma uzoefu wa walimu na wataalamu waliopo zanzibar kwa kuwa zanizbar kulikuwa na wataalamu wa fani mbali mbali wa dini ya kiislamu.
Maalim Seif aliyasema hayo huko Tomondo Wilaya ya Magharibi Unguja wakati akiifungua madrasa hiyo jana jioni ambapo amefahamisha kuwa vijana wa kizanzibari wameacha maadili yao na kuingia katika kutumiya madawa ya kulevya ambayo huwageuza kuwa wezi, wanzinifu na kufnaya vitendo vya vibaya vya kila aina jambo ambalo linatoa taswira mbaya kwa taifa.
“Chuo hichi ni chetu sote tushirikiane na waalimu ili kuona kinapata mafaniko na kufikia lengo letu tulilolikusudia kwa kutoa michango inayohitajika, zanzibar ni sehemu inayojulikana kwa Afrika Mashariki katika kutoa elimu ya dini ya kiislamu kwa hivyo tuendee kutafuta elimu nakuitoa kwa vijana wetu ili hadhi ya zanzibar irudi kama zamani, vijana hawa wanapaswa kuendelezwa ili wawe watoto wazuri wenye kufuata maadili ya dini ya kiislamu ili na wao wakija kuwa wakubwa waweze kutoa elimu kama hii ” alisema Maalim Seif.
Amesema tatizo la madawa ya kulevya ni janga la familia nyingi hivyo ametoa wito kwa jamii kuamka na kuwashughulikia watoto wao ipaswavyo sambamba na kuwapa taaluma ya dini yao na malezi mema ili watoto waepuke kujiingiza katika vitendo viovu na badala yake washughulikie masomo yao.
Maalim Seif amesema jambo jengine ambalo huwa kumba vijana kwa kuacha maadili ni ukimwi ambao umechukua vijana walio wengi na kupunguza nguvu kazi katika familia na Taifa kwa ujumla na kutoa wito kwa vijana kujiepusha na kujiingiza katika vitendo hivyo kwani huleta hasara katiika dunia na akhera.
Seif ameongeza kwa lazima watu wawe wakweli sababu kubwa ya ukimwi ni zinaa ambayo dini yetu inaikemea kwa mujibu wa Quran Tukufu na vitabu na hadithi za mtume lakini kutokana na kushuka kwa maadili watu wamezama katika vitendo hivyo amabvyo mwisho wake ni mbaya sana
“Lazima tuwe wa kweli sababu kubwa ya ukimwi ni kufanya zinaa ambayo dini yetu ya kiislamu inapinga jambo hilo na katika vitabu vya dini vinakatazwa vitendo viovu lakini hivi sasa vijana wetu wamejiingiza sana katika vitendo hivyo …natoa wito kwa walimu kushirikiana na wazee kuhakikisha watoto wetu wanakuwa katika mazingira na malezi ya kiislamu ili kuepusha balaa la matatizo kama haya nchini kwetu” alisisitiza Maalim Seif
Amesema Zanzibar iliyojulikana kwamba ndiyo kitovu kikuu cha kusomea masomo ya dini ya kiislamu ambapo nchi nyingi zilikuwa zinatuma watu wake kuja kupata elimu hiyo, huku akitoa mfano wa Kenya, Uganda, Zambia, Burundi na Malawi vijan wao wengi wamekuja kujifunza hapa nchini.
“Ilikuwa Mzanzibari popote atakapo kwenda Duniani kwenye sherehe za kidini anapewa uongozi kutokana na historiya ya nchi yake, tulikuwa tukisifikana kote ulimwenguni kwa ustaarabu kwa kufuata maadili ya dini ya kiislamu na kwa usomi pia lakini sasa sifa hii imepotea kabisa kwa kuacha maadili yetu, sasa ni wakati wa kurudi tulipotoka katika kufuata maadili yetu na kuirejeshea hadhi yake zanzibar”.alisisitiza Maalim Seif
Mwalimu mkuu kwa upande wake alimfahamisha makamu wa kwanza kwamba madrasa yake inafundisha masomo mbali mbali ikiwemo Quraan Tartili, Tahfidh, Fikih, lugha ya kiarabu na kutoa masomo mengine ya skuli kwa njia ya ziada ikiwa kama kuwasaidia wanafunzi.
Nao wanafunzi wa maadrasa hiyo kwa kupitiya wasomaji risala wamemuomba Makamo huyo wasaidiwe pesa ambazo zitasaidia kununua jengo jengine kubwa kwani kwa sasa madrasa yao tayari inazidiwa na wanafunzi na chuo pekee haikiwezi kumudu gharama hizo.
Kati ya vitu ambavyo wanafunzi hao wamemuomba makamu wa kwanza wa rais ni pamoja na kompyuta na mashine ya photocopy kwa sababu wanapata tabu wakati wa kuchapisha vitabu kwa ajili ya kufundishiya ,hulazimika kutoa pesa nyigi wanapokwenda sehemu nyegine kufuata huduma hiyo.
Wanafunzi hao wamesema vitu vyengine ambavyo ni changamoto katika madarasa hiyo ni vikalio jambo ambalo ni tatizo sugu katika maadrasa hiyo ambapo wanafunzi wanalazimika kukaa chini kutokana na ukosefu wa vikalio.
Katika shrehe hizo Makamu wa kwanza aliahidi kuchangiya shilingi laki tano kwa ajili ya kuboresha maendeleo ya maadrasa hiyo na kuwataka walimu kufanya kazi kwa moyo safi kwani hiyo ni kazi tukufu iliyofanywa na mitume katika kufikisha ujumbe kwa watu mbali mbali ambapo malipo yake watayakuta huko akhaera wenzako.
Madrasa ya Kadiria Immani iliazishwa mwaka 1993 na wanafunzi wa nne ambapo hadi leo imefiksha wanafunzi 250 ikiwa na wanafunzi wanaume 120 na wanafunzi wa wanawake 130. Madrasa hii haifundishi masomo ya kidini tu bali hufundisha kiingereza, kijarumani ,kifaransa na masomo yote ambayo hufundishwa katika maskuli

No comments:

Post a Comment